Beki huyo ameonyesha kuwa ni hodari wa kucheza mipira ya kichwa kwa kuzuia na kushambulia kutafuta mabao kama kona na krosi ingawa wasiwasi uliopo kwa mashabiki wa klabu hiyo ni udogo wa umbile lake.
UKIMUONA umbo lake unaweza kumuona wa kawaida sana, ni umbo
ambalo halitishi. Si mrefu sana, si mpana sana ni mchezaji wa wastani
tu, lakini shughuli yake isubiri uwanjani.
Mmoja wa wachambuzi mahiri na Mhariri wa Michezo
wa Gazeti Kuu nchini Uganda la New Vision Fred Kaweesi alipoisoma
Mwanaspoti na kusikia beki Samweli Ssenkoomi amesaini Simba alitamka
maneno machache; “Simba wamepata mtu, huyo jamaa mzuri sana ila wasimpe
presha bado mdogo sana. Wampe nafasi atumie akili yake.”
Simba imemsajili beki huyo wa Uganda kutoka URA
kwa mkataba wa miaka miwili kwa lengo la kuimarisha safu ya beki ya kati
ambayo iliyumba msimu uliopita na hata kwenye ripoti yake kocha
aliyeachana na Simba, Mfaransa Patrick Liewig alishauri asajiliwe beki
wa kati mzoefu. Alitua nchini usiku wa Jumatatu akitokea kwao Uganda na
kuanza mazoezi ya pamoja na Simba Jumanne jioni wiki hii.
Akiwa katika mazoezi hayo, Ssenkoomi ameonyesha
kuwa ni mjanja uwanjani na ana uamuzi wa haraka na uwezo mkubwa wa
kupanda kushambulia mbele, pia ni mwepesi wa kushuka kuzuia.
Beki huyo ameonyesha kuwa ni hodari wa kucheza
mipira ya kichwa kwa kuzuia na kushambulia kutafuta mabao kama kona na
krosi ingawa wasiwasi uliopo kwa mashabiki wa klabu hiyo ni udogo wa
umbile lake kwa sababu hamtishi straika ila ana akili na anajua
anachokifanya.
Mwanaspoti ilizungumza naye akasema; “Nimeamua
kuja Simba kwa lengo moja la kutimiza kile wanachokikusudia kwa
kuhakikisha nacheza kwa ubora na kuifanya timu ing’are,”anasema
Ssenkoomi ambaye anaishabikia klabu ya Real Madrid ya Hispania
inayofikiria kumpa ukocha Zinedine Zidane.
“Lakini pia kwangu ni hatua moja, nina malengo ya
kucheza Ulaya, kuja kwangu Simba nafungua njia kwa ajili ya kukamilisha
ndoto zangu hizo. Naamini nitafanya kile ninachokikusuadia tena kizuri
zaidi kubwa nahitaji ushirikiano kutoka kwa wachezaji wanzangu, benchi
la ufundi na mashabiki kwa ujumla,”anafafanua Ssenkoomi aliyeweka wazi
tayari amesaini mkataba wa miaka miwili na hakuja Tanzania kukaa benchi
kwavile anataka kung’ara zaidi ya Joseph Owino beki wa Uganda
aliyeondoka Simba.
Hata hivyo Ssenkoomi ametoa angalizo kwa kuwaomba
mashabiki wampe muda kwani anatoka kwenye mapumziko na hajafanya mazoezi
kwa kipindi kirefu.
“Ninatoka kwenye mapumziko, sijacheza kwa kipindi
kirefu, ni ugumu ambao unanitatiza hata hivyo nitafanya kitu
kitakachowafurahisha benchi la ufundi na mashabiki kwa ujumla,”anasema
mchezaji huyo ambaye baada ya mazoezi ya kwanza na Simba alilalamikia
uchakavu wa Uwanja wa Kinesi, Dar es Salaam.
“Kitu kingine ni ubovu wa sehemu ya kuchezea
ndani, hali ya uwanja si nzuri imekuwa ikinipa wakati mgumu kucheza.
Ushindani upo kila mahali, nimefurahi kukutana na wachezaji mbalimbali
na kwa kipindi kifupi nimependa ushirikiano wao,”anasema na kuongeza
kuwa amezoea mazingira ya Afrika Mashariki hivyo hadhani kama Tanzania
itampa shida kwavile haitofautiani na Uganda.
“Wachezaji wazuri ambao kwangu ni changamoto na
mambo mengine ni mimi mwenyewe katika kujituma, kufahamu majukumu yangu
ninayopewa na mwalimu,” anaongeza mchezaji huyo ambaye Mwanaspoti
linajua amependekezwa na Mkurugenzi wa Ufundi wa Simba, Mosses Basena
ambaye ni raia wa Uganda.
Basena amewaambia viongozi kwamba mchezaji huyo ni
mzuri na anaweza kufanya kazi kubwa kwenye ufundi ingawa habari za
ndani zinadai kiungo wa TP Mazembe, Patrick Ochang anaomba kila kukicha
arudi Msimbazi baada ya kupoteza namba katika kikosi cha wachezaji 18 wa
kwanza Mazembe hivyo kumfanya kupoteza posho na masilahi manono.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni